Jumanne, 23 Januari 2024

KUSAMEHE, MSAMAHA Na Christopher Mwakasege

 Felix Mbwanji:

SAMEHE NA KUSAHAU (BY MWL, C.MWAKASEGE)

                            

TABIA YA MUNGU YA KUSAMEHE NDANI YAKO

         Ulipompokea Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yako, ulipokea tabia ya aina gani?

"  Bali wote waliompokea (Kristo) aliwapa uwezo wa  kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake; waliozaliwa, si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili, wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa Mungu." (Yohana 1:12,13)


         Ulipozaliwa mara ya pili kwa Neno la Kristo ulifanyika kuwa mtoto wa Mungu.

Watoto wa Mungu wana tabia ya namna gani?

         Kwa kuwa wamehamishwa toka ufalme mwingine na uzazi mwingine, na kuingizwa katika ufalme wa Mungu na uzazi wake (Wakolosai 1:13); watoto hawa wanatakiwa wawe na tabia nyingine.


          Kabla ya kuzaliwa mara ya pili, kabla ya kumkiri Kristo ya kuwa ni Bwana: ulikuwa na tabia ya dunia hii iliyoongozwa na mfalme wa dunia hii ambaye ni shetani.

          Ulipozaliwa mara ya pili na kuukiri wokovu katika Kristo, ulipokea tabia mpya inayoongozwa na Mungu mwenyewe aliye ndani yako.


"  Kwa kuwa uwezo wake wa Uungu umetukirimia  vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa (Utakatifu), kwa kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe. Tena kwa hayo ametukirimia ahadi kubwa mno; za thamani,ili kwamba kwa hizo mpate kuwa Washirika wa TABIA YA UUNGU, mkiokolewa na uharibifu uliomo duniani kwa sababu ya tamaa." (2 Petro 1:3,4)

          Mistari hii inatuonyesha wazi kabisa kuwa kwa uweza ule ule uliokuwezesha kuwa mwana wa Mungu, unakuwezesha kuipokea tabia ya Mungu.

          Tabia ya Mungu iliyo wazi ni Upendo kwa kuwa Mungu ni Upendo

(1 Yohana 4:8)


          Ni upendo ambao huvumilia, hufadhili, hauhusudu, hautakabari, haujivuni, haukosi kuwa na adabu, hautafuti mambo yake, hauoni uchungu, hauhesabu mabaya, haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli,huvumiliayote,huamini yote, hutumaini yote, hustahimili yote, haupungui neno wakati wowote.Kamailivyoandikwa katika (1 Wakorintho 13:4 - 8)

 Mungu anavyosamehe:


      Ndani ya upendo, kuna tabia ya kusamehe na kusahau. Ili kuifahamu zaidi na tuitafakari tabia ya Mungu ya kusamehe na kusahau. Mungu anasema hivi:

"  Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe; wala sitazikumbuka dhambi zako." (Isaya 43:25)


Na tuitafakari tabia hii ya Mungu katika mafungu mawili yafuatayo:


1. Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe; na;

2. Wala sitazikumbuka dhambi zako.


           Haya ni maneno ya Mungu ambayo aliyasema kwa kutumia kinywa cha nabii Isaya, kwa ajili ya watu, baada ya kufunga agano jipya katika damu ya Yesu Kristo pamoja nao. Kwa kuwa katika agano la kale makosa (au dhambi) yalikuwa hayafutwi ila yanafunikwa tu kwa damu ya wanyama waliotolewa sadaka (Waebrania 10:1 - 25)


          Lakini katika agano jipya, makosa yanafutwa kwa uwezo wa damu ya Yesu iliyomwagika msalabani.

          Kuna tofauti kubwa kati ya kuifunika dhambi kwa damu na kuifuta dhambi kwa damu. Unapofunika, kosa haliondoki linabaki pale pale, lakini linakuwa halionekani. Unapofuta, kosa linaondolewa kabisa, inakuwa kama hakuna kosa lililowahi kufanyika.


          Ukiwa darasani, mwalimu akifuta maandishi ya chaki ubaoni, ubao unabaki hauna maandishi; unakuwa safi. Lakini utakuta yale yaliyokuwa yameandikwa, ingawa hayapo ubaoni, katika akili za watu yanakuwa yapo. Na wakati mwingi inachukua muda kufutika mawazoni.

          Sasa, ile sehemu ya kwanza ya mstari, Mungu anasema anayafuta makosa yetu kwa ajili yake mwenyewe, Mungu hakusema "Anayafunika makosa," bali amesema, "anayafuta makosa".

Soma tena:

"Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe."

Soma na maneno haya:

"Tukiziungama dhambi zetu, yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote" (1Yohana 1:9)


         Ukitubu dhambi zako kwa Mungu katika Roho na Kweli, Mungu anakusamehe, na anafuta dhambi zako na mbele yake unaonekana kama hukufanya kosa lo lote. Hivyo ndiyo maana ya kuhesabiwa haki mbele za Mungu katika Kristo. Kusamehe ni kufuta au kuondoa kosa na kulisahau au kutokulikumbuka tena.

 Kusamehe kosa = kufuta + kutokulikumbuka kosa

         Wakati huu tunatizama jinsi Mungu anavyotusamehe. Hatua ya kwanza anafuta kosa machoni pake.

          Kwa nini Mungu atusamehe?

          Kwa nini Mungu ayafute makosa yetu?

          Umewahi kujiuliza kwa nini Mungu aliamua kukusamehe mabaya yote uliyoyafanya maishani mwako?

          Watu wengine wanafikiri wokovu unakuja kwa kumpendeza Mungu kwa matendo yao. Na matokeo yake wanajihesabia haki wenyewe badala ya kuhesabiwa haki na Mungu.


          Utamsikia mtu anasema mimi sina dhambi, siibi, sizini, silewi, sijatengwa na kanisa, na naitunza Sabato kwa hiyo sina kosa kwa Mungu!

 Lakini neno la Mungu linatuambia mambo tofauti, kwa mfano neno linasema hivi:


" Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala SI KWA MATENDO, mtu awaye yote

 asije akajisifu (Waefeso 2:8,9)


         Kwa hiyo, unaona kuwa matendo yako peke yake hayawezi kukupa wokovu, na ondoleo la dhambi, bila ya imani ndani ya Kristo. Imani lazima iambatane na matendo. Imani pasipo matendo imekufa (Yakobo 2:26).

         Kitu kinachomfanya Mungu akusamehe si uzuri wa matendo yako; bali anakusamehe KWA AJILI YAKE MWENYEWE.

           Mungu anasema; "Mimi, naam, Mimi, ndimi niyafutaye makosa yako KWA AJILI YANGU MWENYEWE"

         Huu ndiyo upendo wa ajabu!

         Kumbuka si kwa matendo yako bali kwa ajili yake mwenyewe Mungu, unapata kusamehewa makosa yako.

Mungu akisamehe anasahau:


         Hatua ya pili ambayo Mungu anaichukua mara tu anapofuta makosa yako ni kuyasahau aliyokwisha yafuta.

         Yeye mwenyewe ameahidi kwamba ".... Wala sitakumbuka dhambi zako". WALA SITAKUMBUKA DHAMBI ZAKO!


         Ina maana kuwa Mungu akiisha kukusamehe kwa ajili yake mwenyewe; anafuta na kusahau makosa uliyofanya, anakuhesabia haki bure mbele zake. Unasimama ndani yake kama mtu ambaye hajawahi kufanya kosa wala dhambi yo yote.

         Sasa kama Mungu amekwishafuta na kuyasahau mambo uliyofanya kabla hujaokoka na ukatubu, kwa nini wewe unayakumbuka? Jifunze kujisamehe mwenyewe! Mungu akikusamehe na wewe jisamehe. Mungu asipoyakumbuka makosa yako, na wewe usiyakumbuke!


         Huduma za watumishi wengi zinakwama mara tu anapokumbuka mambo aliyoyafanya zamani au maneno aliyoyasema - hata kama wamekwishayatubia!

         Kwa sababu hiyo, badala ya kusonga mbele katika Bwana, anajikuta kila wakati wanatubu juu ya dhambi hiyo hiyo. Na wanakosa ujasiri wa kusimama mbele za Mungu, mbele ya shetani na mbele za watu.


         Kila wanapotaka kufanya kitu, shetani anawaletea wazo kuwa, bado hawajasamehewa kosa alilolifanya jana au juzi. Na kwamba haitakuwa rahisi kwako kupokea baraka toka kwa Mungu. Kwa hiyo watu hawo anaanza kutubu tena upya!

         Watu wengi hata sasa hawana uhakika kama Mungu amewasamehe juu ya makosa waliyoyafanya.

         Uhakika utaupata katika Neno la Mungu.

Mungu ameahidi kuwa ukitubu katika Roho na Kweli, unasamehewa.

(1Yohana 1:9)


         Paulo alifahamu siri hiyo ya kuyasahau mambo ya nyuma aliyomkosea Kristo, kwa kuwatesa wafuasi wa Yesu, kabla ya kuokoka kwake. Hii ilimsaidia kulitangaza Jina la Yesu bila yeye kujisikia vibaya moyoni mwake.

Kwa hiyo Paulo aliweza kusema:


"...... ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele, nakaza mwendo niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu" (Wafilipi 3:13,14)

            Ili uweze kusonga mbele katika wokovu, ni budi ujifunze kujisamehe na kuyasahau uliyoyafanya zamani.

Tabia hii unayo ndani yako:


         Kuyafuta makosa na kutoyakumbuka tena ni tabia ya Mungu ambayo imo ndani yako sasa.

         Ulipompokea Kristo moyoni mwako na kumkiri kuwa ni Bwana wa maisha yako, pia ulipokea ndani ya moyo wako tabia hii ya Mungu ya kufuta makosa na kutoyakumbuka.

         Hii ndiyo tabia inayotakiwa ionekane katika maisha yako unapokosewa na mtu.


         Tatizo la wengi ni kwamba wamekuwa viumbe vipya, lakini wanataka kutumia tabia yao ya zamani. Katika tabia ya zamani, walisamehe lakini hawakusahau walichokosewa. Tabia mpya ni kufuta makosa na kutoyakumbuka kabisa. Kwa hiyo na sisi tukikosewa tunatakiwa kusamehe na kusahau!

Hatua zifuatazo katika mfululuzo wa masomo yanayofuata wiki zijao zitakusaidia kuijenga na kuitumia tabia hiyo ya Mungu iliyo ndani yako. Tunaamini utakuwa pamoja nasi wiki ijayo ili kuendelea na somo hili - katika kipengele kinachosema: "Hasara za kulipiza kisasi"


HASARA ZA KULIPIZA KISASI

         Usilipize Kisasi! Unasikia? Hata ikiwa umefanyiwa ubaya wa namna gani, Biblia inafundisha na inakusihi usilipize kisasi kwa huyo aliyekufanyia ubaya. Biblia inasema hivi:


"Wapenzi, msijilipizie kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, kisasi ni juu yangu Mimi, Mimi nitalipa, anena Bwana" (Warumi 12:19)


         Kuna hasara zinazoweza kukupata ukiamua kulipa kisasi kwa mambo uliyofanyiwa ambayo hayakupendezi. Ikiwa ni masuala ya kikabila, usilipe kisasi. Ikiwa ni masuala ya kidini, usilipe kisasi. Ikiwa ni masuala ya kifamilia, usilipe kisasi. Ikiwa ni masuala ya kikazi, usilipe kisasi. Ikiwa ni masuala ya uhusiano wako na majirani zako, usilipe kisasi.Ndiyo! Usilipe kisasi! Kwa nini? Kwa sababu "imeandikwa kisasi ni juu yangu Mimi; Mimi nitalipa, anena Bwana".

Lakini ikiwa utaona ya kuwa Mungu hawezi kukusaidia na ukaamua kujichukulia madaraka ya kujilipiza kisasi hasara zifuatazo hakika zitakupata!


Hasara ya Kwanza:

UTASHINDWA!

         Katika jambo lolote lile lililokukasirisha - liwe la kidini, au kikabila, au kifamilia, au kikazi, na kadhalika ukiamua kulipa kisasi utashindwa wewe kwa sababu vita hivyo si vya mwili na wala silaha ambazo Mungu amekupa si za mwili! Tunasema hivi kwa sababu katika 2 Wakorintho 10:3- 5 imeandikwa hivi:"Maana ingawa tunaenenda katika mwili, hatufanyi vita kwa jinsi yamwili; maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome, tukiangusha mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara kila fikra ipate kumtii Kristo".


         Tena katika kitabu cha Waefeso 6:12 imeandikwa hivi: "Kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho".

         Uwanja wa mapambano uliyonayo ni "katika ulimwengu wa roho" na mapambano uliyo nayo "si juu ya damu na nyama" - ingawa unaona ya kuwa ni watu na ni binadamu kama wewe wanaokusonga - lakini fahamu hili ya kuwa wanatumiwa tu na ibilisi!

         Mbinu mojawapo ya shetani anayotumia akitaka kukuangamiza ni kukufanyia kitu kitakachokukasirisha ili uamue kujibu au kushindana kimwili kwa sababu anajua ukishindana "kimwili" au katika mwili utashindwa hakika, maana vita hivyo si vya mwili wala silaha ambazo Mungu amekupa si za mwili!


Hasara ya Pili:

MATATIZO HAYATAKWISHA!

         Kumbuka imeandikwa hivi katika kitabu cha Wagalatia 6:7; "Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa chochote ampandacho mtu. Ndicho atakachovuna".

         Ikiwa umeamua kulipa kisasi kwa kumfanyia ubaya yule aliyekufanyia - ubaya hautakwisha, kwa sababu utavuna ulichopanda.Ndiyo maana imeandikwa hivi:"Yeye arudishaye mabaya badala ya mema, mabaya

hayataondoka nyumbani mwake" (Mithali 17:13)

         Ukiamua kulipiza kisasi kwa kumfanyia ubaya yule wa nyumbani mwako - Biblia inasema "mabaya hayataondoka nyumbani mwako" Hii ndiyo maana matatizo mengi katika ndoa na katika jamii hayaishi - kwa sababu mtu akifanyiwa ubaya naye analipa kisasi.

         Ukiamua kulipa kisasi kwa kumfanyia ubaya yule wa nchini mwako ujue hakika mabaya hayataondoka nchini mwako. Hili ndilo lililowapata wenzetu wa nchi za Burundi na Rwanda - kulipizana kisasi - matokeo ni uhasama usiotaka kupotea - pamoja na juhudi zote za kimataifa kutafuta suluhisho.

         Ukiamua kulipa kisasi kwa kumfanyia ubaya yule wa kazini kwako - fahamu mabaya hayataondoka kazini kwako. Ikiwa ni shuleni - mabaya hayataondoka hapo shuleni.

         Tena hali ya mwisho inakuwa mbaya zaidi,kila wakati kisasi kinapoendelea kupandwa. Kwa sababu ukiwapa watu ubaya - nawe utapewa ubaya kwa; "kipimo cha kujaa na kushidiliwa, na kusukwa - sukwa - hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile upimacho ndicho mtakachopimiwa (Luka 6:38)

         Kumbuka ubaya haushindwi na ubaya mwingine, bali unashindwa na wema - kama vile dawa ya chuki si chuki bali upendo! Ndiyo maana Warumi 12:21 inasema; "Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema".


Hasara ya Tatu:

UNAMZUIA MUNGU KUKUPIGANIA

         Unaweza ukashangaa, lakini ndivyo ilivyo! Ukiamua kulipa kisasi juu ya tatizo ulilonalo - unamzuia Mungu asikusaidie kulitatua.Mungu hawezi kukusaidia kwa sababu imeandikwa "msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana, imeandikwa, kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana".

Neno "ipisheni" limeandikwa kwa sababu kulipa kisasi "kunazuia" ghadhabu ya Mungu isipigane upande wako! Tena si hivyo tu lakini ukilipa kisasi unaingilia kazi ambayo si yako! Ni kazi ya Mungu maana anasema "Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana" Ikiwa kisasi ni juu ya Mungu kulipa, basi huhitaji wewe kulipa. Je, tunakwenda pamoja katika hili?

         Hatua yako ya kulipa kisasi inazuia mkono wa Mungu kukupigania - kwa hiyo ipishe ghadhabu ya Mungu kwa kutokujilipizia kisasi!


Hasara na Nne:

UNAJICHUMIA DHAMBI!

         Unapoamua kulipa kisasi, unajichumia dhambi! Hii ni kwa sababu kulipa kisasi huja kwa njia ya chuki iliyojengeka ndani yako kwa ajili ya mambo mabaya uliyofanyiwa. Huwezi kulipa kisasi bila ya kumchukia huyo unayejilipizia kisasi kwake. Na Biblia inasema hivi:


"Kila amchukiaye ndugu yake ni mwuaji: nanyi mnajuaya kuwa kila mwuaji hana uzima wa milele ukikaa ndani yake" (1 Yohana 3:15).

Umeona hilo! Chuki huzaa kisasi, na huzaa dhambi ya kuua! Na

Isaya 59:2b inasema; "dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia".


         Kwa hiyo kama umekwisha lipa kisasi au umekusudia moyoni mwako kulipa kisasi ni muhimu utubu ili Mungu akusamehe na mawasiliano yako na Yeye yawe mazuri.

Usikose kusoma wiki ya nne ya mfululizo huu tutakapojifunza juu ya:

Hatua tano Muhimu katika kusamehe na kusahau


JE ALIYEKUKOSEA ASIPOKUOMBA MSAMAHA UFANYEJE?


"Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwana neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu.Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu" (Marko 11:25,26)


         Yesu Kristo aliyasema maneno haya kwa wanafunzi wake wa kwanza, alipokuwa akiwafundisha juu ya imani. Maneno haya ya Yesu Kristo, yanatuhusu hata sisi tulio wanafunzi wake siku hizi.Yesu Kristo katika maneno haya anazungumza na mwanafunzi wake aliyekosewa na mtu mwingine.Na katika somo hili, toka mwanzo tumechukua mtazamo huu wa Yesu Kristo; tunazungumza na mtu aliyekosewa na mtu mwingine.Somo hili lina maneno yenye mafundisho kwa mtu ambaye amekwazwa na mwenzake;mtu aliyefanyiwa kosa lolote lile.Kuna watu wengi sana wanaokosewa na watu wengine. Na tunaamini hata wewe kuna wakati fulani katika maisha yako umekwazwa na mtu mwingine.Katika ndoa makwazo yamekuwa kitu cha kawaida. Maofisini watu wanakosana kila siku. Hata na katikati ya watu wa Mungu, makwazo yanatokea mara kwa mara.Na sehemu mojawapo muhimu katika maisha ya mkristo ni maombi. Na ili tuwe na maisha ya maombi yenye mafanikio, ni lazima tuwe watu wenye tabia ya kusamehe waliotukosea.Yesu Kristo alijua jambo hili na umuhimu wa kusamehe KWANZA kabla ya kuanza kuomba.Yesu Kristo alisema, " Ninyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu".Maneno haya hayatupi uchaguzi wa kusamehe mtu wakati tunapopenda tu au wakati tunapotaka.Maneno haya ni agizo la Bwana Yesu Kristo ambalo linatakiwa lifuatwe na kila mwanafunzi wake, ili aweze kuwa na mafanikio katika maombi yake.


Unatakiwa kusamehe mara ngapi?

         Mama mmoja ambaye alikuwa ana matatizo katika unyumba wake, alisikika akisema maneno haya:"Mume wangu amenitesa kwa muda mrefu sasa; na hali ya mambo ilivyo, sidhani kama naweza hata kumsamehe tena; maana nimemsamehe nimechoka".Ni kweli kabisa kwamba mtu mwingine anaweza kukukosea mara nyingi sana. Hii huwa mara nyingi inatokea kwa watu ambao wanakaa pamoja au ni majirani.Hali ya mama huyu aliyesema maneno hayo, inawapata watu wengi sana, na nina uhakika watu hao wamechoka na hali hiyo.


         Inawezekana wewe ni mke wa mume ambaye ni mlevi, malaya, na mgomvi. Kila akirudi nyumbani ni kukutukana na hata wakati mwingine kukupiga. Na umeomba kwa Mungu juu ya jambo hili kwa muda mrefu bila kuona mafanikio.Sasa umeamua ufanyaje wakati unaona unazidi kuonewa na kuteswa? Inawezekana wewe ni mume wa mke ambaye ni mlevi, malaya na mgomvi. Inawezekana wewe ni mzazi wa watoto ambao hawakusikii, walevi, malaya, na wahuni.Inawezekana wewe ni mfanyakazi katika ofisi ambayo unaonewa haki zako za kupanda cheo, kupanda mshahara na marupurupu mengine, bila sababu yoyote.Sasa, nakuuliza, umeamua kuwachukulia hatua gani hao watu waliokukosea?Kumbuka wewe ni mkristo, na unatakiwa uamue mambo yako kikristo, kwa kulifuata Neno la Mungu.Hawa watu wanaotukosea tunatakiwa kuwasamehe mara ngapi? Hili swali ni muhimu, kwa kuwa watu wengine hawachoki kuwakwaza wengine!


Imeandikwa:"Jilindeni; kama ndugu yako akikosa, mwonye;akitubu msamehe. Na kama akikukosa mara saba katika siku moja, na kurudi kwako mara saba,akisema, Nimetubu, msamehe" (Luka 17:3,4):


         Ni kweli kabisa! Mtu akikukosea na akitubu ni rahisi kumsamehe. Lakini ikiwa mtu aliyekukosea asipokuja kutubu je naye anahitaji kusamehewa?Hata asipotubu msamehe.Hili ni jambo ambalo inabidi tulizungumze kwa kufuata Neno la Mungu; maana ni jambo linalowasumbua wengi.Kuna wakati fulani tulikuwa tunalijadili jambo la kusamehe na wenzetu. Mmoja kati ya wale waliokuwepo alisema hivi: "Mimi siwezi kumsamehe mtu aliyenikosea asipokuja kutubu".Inawezekana hata wewe una mawazo kama haya. Lakini nakuuliza swali hili, "Je, kuna mstari wo wote katika biblia unaosema mtu aliyekukosea asipotubu usimsamehe?".


         Sisi hatujawahi kuuona. Kama upo tunaomba utuambie.Huhitaji kuombwa msamaha ili upate kusamehe. Biblia inasema; ‘Utusamehe deni zetu, kama sisi tuwasamehevyo wadeni wetu’ Biblia haikusema ‘Utusamehe deni zetu, kama sisi tuwasamehevyo waliotuomba msamaha!Kwa hiyo tunatakiwa kuwasamehe waliotukosea hata kama hawakutuomba masamaha.Hii ni kweli. Na sasa tuone neno la Mungu linatuambia nini:


"Kisha Petro akamwendea akamwambia, Bwana,ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba? Yesu akamwambia, si kuambii hata mara saba,bali hata saba mara sabini" (Mathayo 18:21,22)


         Hapa hatuoni Yesu Kristo akimwambia Petro kuwa mtu ni lazima atubu ili asamehewe. Ila anamjibu kuwa "Sikuambii hata mara saba, bali saba mara sabini"Petro alifahamu ya kuwa anahitaji kusamehe hata asipoombwa msamaha. Tatizo lake lilikuwa ni asamehe mara ngapi.Kumbuka ya kuwa unayaweza mambo yote, pamoja na kusamehe bila kuombwa msamaha, katika yeye akutiaye nguvu (Wafilipi 4:13) Tena kumbuka ya kuwa ni tabia ya Mungu iliyo ndani yako (2Petro 1:3,4) inayokuwezesha kusamehe na kusahau hata kama hujaombwa msamaha.Kumbuka si wewe unayekosewa na kukwazwa, bali Kristo aliye ndani yako. Kwa kuwa ulipompokea Kristo katika moyo wako, ulifanyika kuwa kiumbe kipya. Si wewe unayeishi, bali Kristo ndani yako (Wagalatia 2:20)


MUNGU ALITUSAMEHE KABLA SISI HATUJAMUOMBA MSAMAHA WALA KUTAMBUA KOSA LETU.MUNGU ALITULIPIA DENI LETU LA DHAMBI KABLA SISI HATUJAMUOMBA MSAMAHA.


Kwa maana imeandikwa: "Bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi" (Warumi 5:8)."…….Kristo alikufa kwa ajili yetu tulipokuwa tungali wenye dhambi". Maana yake tulipokuwa bado hatujaomba msamaha Yesu alikufa kwa ajili yetu. Mshahara wa dhambi ni mauti (Warumi 6:23). Na kwa kufa Kristo inamaanisha tumesamehewa na kulipiwa deni letu. Kazi tunayotakiwa kuifanya ni kuupokea msamaha kwa njia ya toba.


         Hata Yesu Kristo alipoteswa na kusulubiwa, na kufa msalabani, aliwasamehe waliomsulubisha na akawaombea msamaha (Luka 23:34); KABLA ya kuombwa msamaha.Na ni sauti ya Yesu Kristo inayosema ndani yako ukikosewa na mtu; "Msamehe kwa kuwa hajui alitendalo". Na Yesu akisema msamehe mtu, basi huna budi kusamehe.Na kumbuka unatakiwa kusamehe KWA AJILI YAKO MWENYEWE, hata kama hujaombwa msamaha ili na wewe usamehewe na Mungu. Usiposamehe unazuia maombi yako yasijibiwe na unazuia baraka zako zingine.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni