Alhamisi, 4 Juni 2020

NGUVU YA MAOMBI YA KUOMBA BILA KUKOMA


Na Mwalimu Oscar Samba:
“Akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa.” Luka 18:1.
Nina kusalimu ndugu yangu kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo! Ni yangu matumaini ya kuwa u mzima tena buheri wa afya tele, na kama sivyo basi Bwana wetu Yesu Kristo aipatie nafsi yako amani, na faraja tele. Na kama ni uponyaji au haja fulani, ipokee kwa imani sasa!
Siku ya leo hapa mtandaoni nimekuandalia ujumbe huu muhimu sana, wenye mukutadha ama sura ya kukutaka kuona umuhimu wa maombi ya nayoombwa bila kukoma, au kukata tamaa!


Kuomba sio msisitizo wangu mkubwa sana hapa, bali ulio mkubwa ni kuomba bila kukuta tamaa, ni maombi yenye kukaza na yasiyo na hali ya kulega, au muombaji asiye zimia njiani, ni mwenye kumngoja Bwana, kama vile Zaburi isemavyo kuwa amemngoja kama vile mlinzi aingojavyo asubuhi, au Ayubu kama vile muajiriwa anavyosubiria mshahara wake wa mwisho wa mwenzi!

Huku siko kungoja kwa kawaida, bali ni kungoja kulikojawa na matumaini ndani yake wapo wanaongoja ila mioyoni mwao walishazimia, maana kitendo cha Zakaria kushindwa kumuamini moja kwa moja malaika Gabrieli aliyemletea taarifa za majibu ya maombi yao kiliashiria hali fulani ya kuchoka au kuvunjia moyo ndani!

Mpendwa! Kisa kifuatacho ni muhimu sana kwenye maisha yako ya wokovu ! ni habari za mtu ambaye Yesu anatufunza kuhusu jambo hili kwamba alikuwa na rafiki yake, na alipatwa na mgeni, na kwenda kuhitaji msaada kwake maana mgeni huyu alikuja usiku na hakukuwa na bajeti yake, naye moja kwa moja kufikiri kwenda kwa rafiki yake ili amsadie!

Alipomuendea haikuwa jambo jepesi kwake kupata msaada, bali moja kwa moja alikabiliaana na upinzani, lakini hakukata tamaa, alizidi kukaza, na hatimae rafiki yake aliamua kumpatia hitaji lake!

Ona:
  Akawaambia, Ni nani kwenu aliye na rafiki, akamwendea usiku wa manane, na kumwambia, Rafiki yangu, nikopeshe mikate mitatu,
  kwa sababu rafiki yangu amefika kwangu, atoka safarini, nami sina kitu cha kuweka mbele yake;  na yule wa ndani amjibu akisema, Usinitaabishe; mlango umekwisha fungwa, nasi tumelala kitandani mimi na watoto wangu; siwezi kuondoka nikupe?  Nawaambia ya kwamba, ijapokuwa haondoki ampe kwa kuwa ni rafiki yake, lakini kwa vile asivyoacha kumwomba, ataondoka na kumpa kadiri ya haja yake.

Yesu anunganisha kisa hiki na somo la kujibiwa kwa maombi yetu, jambo linalotupa hakikisho la kujibiwa ila changamoto inasalia kuwa ni kuwa na aina hii ya moyo au tabia ya kutokukata tama kabla ya kupokea majibu yetu!
Endelea kusoma: Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa. Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe au samaki, badala ya samaki atampa nyoka? Au akimwomba yai, atampa nge? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao? Luka 11:5-13.

Ni kwambie wazi kuwa sio kila mahitaji utayapata kwa wakati ambao wewe unautaka, na ni kawaida kabisa ya moyo wa mwanadamu kuumia pale mahitaji yanaposhindwa kupatikana au kupatiwa ufumbuzi kama muhusika alivyohitaji, maana Mithali husema bayana kuwa hiyo haja ikipatikana ni kama mti wa uzima ila ikikosekana moyo huugua, 13:12, lakini nakuimiza sana kufahamu kuwa sio kila hitaji uombalo utajibiwa kiwepesi, na kimya cha Mungu haimaanishi kuwa amekusahau, au amepuzia hitaji lako! Hili lishike sana.

Sasa leo sitakujuza sababu za Mungu kutokufanya hivyo, ila tambua kwamba zipo kadha wa kadha ikiwemo za Mungu kukuimarisha kiroho, akihitaji kukujengea saburi, na kisha udhabiti wa moyo kama vile Warumi 5:1-5 inavyodhibitisha, lakini usisahau kwamba upinzani pia upo, majibu ya muombaji Danieli yalichelewa na ni shauri ya upinzani, nawe yamkini siku uliyoanza kuomba tu ulikwisha kujibiwa ila adui ameweka upinzani, sasa usife moyo bali endelea kuomba yamkini upo siku ya 20 au ya 17, na bado masaa au siku chache tu ili upokee mujiza wako!

Najifunza nguvu hii ya maombi ya kutokukata tamaa sio kwa Danieli tu ambaye licha baada ya kumaliza siku zake 21 alikuja kutokewa kiupya na Mungu siku ya 4 baada ya kumaliza hiyo vita, lakini pia ninaipata nguvu na ujasiri mwingine ninao uchukuwa kutokana na mafunzo ya Yesu katika kitabu kile cha Luka 18, pale tunajifunza funzo muhimu sana, ambalo linatutaka sio kusalia na matumaini tu, bali tuendelee kumkumbusha Mungu, japo haina maana kuwa huwa anafika pahali na kusahau, ila kumkumbusha kwetu ni sawa na kumsonga, kama huyu mjane kwa hakimu, ama kama vile huyu aliyemwendea rafiki yake na kuzidi sana kumsonga, kisha alipokea haja yake!

Ni kweli Mungu huweza kusema nitakujibu, nitakupa, ila kwa kumsonga kwako akalifanikisha kwa haraka, na ipo hatari kwamba kwa kunyamaza kwako huwenda usilipate kabisa jambo hilo, maaana jaribu kufikiri kama huyu angeishilia hatua ya kwanza mara baada ya jibu la rafiki yake kuwa tumekwisha kulala na hakuhitaji huo usumbufu ama jibu la awali la hakimu kama lingefanyika kikwazo kwa mama mjane! Sidhani kama hitaji lao lingalikuwa na majibu!
Jionee:
     Akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa. Akasema, Palikuwa na kadhi katika mji fulani, hamchi Mungu, wala hajali watu. Na katika mji huo palikuwa na mwanamke mjane, aliyekuwa akimwendea-endea, akisema, Nipatie haki na adui wangu.
Naye kwa muda alikataa; halafu akasema moyoni mwake, Ijapokuwa simchi Mungu wala sijali watu, lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa kunijia daima. Bwana akasema, Sikilizeni asemavyo yule kadhi dhalimu. Na Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao? Nawaambia, atawapatia haki upesi; walakini, atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani?

Jambo hili na aina hii ya tabia ni muhimu sana katika maisha ya muamini! Usikubali kuwa mtu mwepesi wa kukata tamaa, maisha ya wokovu yanawahitaji mashujaa wa imani, watu ambao wanaona majibu hata katika mazingira ambayo sio rahisi kuonekana, uwe kama Daudi, wakati wengine wamekata tamaa, na hawauoni msaada wa Mungu maana adui yao amewatukana kwa muda wa siku 40, yeye aliuona, na kusema kuwa asizimie mtu moyo, tena amwambia mfalme Sauli, ikiwa na maana kwamba alimjua anayemtegemea na kumuamini.

Uwe shujaa wa imani, usikubali kuchoka kiwepesi, macho yako yamtazame yeye, mkumbuke mwanamke aliyeshika pindo la Yesu, na kupokea uponyaji wake ni kwamba aliteseka na jambo hilo kwa muda wa miaka 12, na baadae Mungu alikuja na kumtokea, lakini hakumtokea akiwa amechoka, bali alichukuwa hatua ya kushika ule upindo, aliungangania na kisha kuondoka na mujiza wake.

Mpedwa kuchoka kiroho hukuondolea imani, kwa hiyo siku ya kushika pindo itakupita maana imani yako haipo tena, na utakuwa ukibishana na msukumo wa Roho Mtakatifu unapokutaka kuingia kwenye maombi, kama walio wengi hivi leo wanavyobishana maana wamechoka, na wanapoimizwa kufunga na kuomba, wanaanza kuwaza na kukubali kuhubiriwa na Shetani kuwa mbona Mungu hakuwatokea siku zote hizo! Huo ni moyo ulioinama na kwa bahati mbaya sana unashindwa kushika pindo la Yesu!

Mpendwa ni kweli swala la kuomba bila kukoma halipo tu katika mukutadha wa muda, (ikiwa na maana ya muhusika kuona majibu yake yamekawia tu la!) Bali hata vikwazo!

Kuna watu wanapanga maombi ya kufunga na kuomba na kukitokea vita wanajikuta wanahairisha, huko ni kushindwa kushinda vizuizi vya maombi, wengine huishilia kufadhaika na kumia kissha kujikuta wakiomba kiulegevu au hawaombi kabisa, na wapo ambao huomba maombi ya manunguniko; mtu mmoja akaniambia kuwa anajikuta kila akitaka kuomba au akimtafakari Mungu anamtukana tu! Ni baada ya kumuona Mungu kama aliyechelewa kumponya dada yake!

Mtu mmoja alisema kuwa Mungu ni Mungu hata kama hajajibu maombi yake, na hata kama amechelewa huwa anasalia kuwa Mungu, amejibu au hajajibu, hiyo haibadilishi Uungu wake! Wala msingi wa Uungu na wokovu haupatikani katika kuomba na kujibiwa!

Hapa ni muhimu sana kupajua maana nimeona watu walioomba ndugu zao wapone na wanapokuja kufariki au kuteseka kwa muda mrefu, hujikuta wanashindwa kumuelewa Mungu hata wengine kufikia hatua kabisa ya kutaka kuacha wokovu, na wengine hawaombi tena, ama hujawa na manunguniko!

Sasa kitabu chetu cha USIFIE JANGWANI kina mada ya namna ya kufanya unapomuona Mungu amechelewa au kukawia kujibu maombi yako, pia kipo kitabu cha NGUVU YA MAOMBI YA MUDA MREFU, lakini fahamu sana kuwa Mungu ni Mungu hata kama amekujibu au hajakujibu!

Daudi alikuwa ni mfalme, lakini aliomba na mwanae hakupona, Yesu aliwahi kuomba maombi ambayo hayakujibuwa, yale ya kikombe kimuepuke, aliwahi kuumia na kufikia hatua ya kusema Mungu wangu mbona umeniacha! Hapo napo pana funzo kubwa!

Lakini tukiendelea ni kwamba, ni muhimu kujifunza kushinda vikwavyo, na vipo vingi, mumeo, au mke, watoto, na afya, mchungaji kwa watumishi, au washirika na wakuu wako kikazi wanaweza kufanyika kikwazo, lakini wewe usife moyo na kuamua kuhairisha maombi yako, au kujikuta ukiomba kwa ulegevu ama kuacha kuomba kabisa!

Jionee kwa huyu mtu! Alikuwa ni kipofu, napo alihitaji kumuendea Yesu. Lakini watu wake Yesu waliokuwa nae, ambao tulitegemea ndio ambao walipaswa kuwa msaada wa kwanza kwake, walimvunja moyo, walijaribu kumzuia!
Wakafika Yeriko; hata alipokuwa akishika njia kutoka Yeriko, pamoja na wanafunzi wake, na mkutano mkubwa, mwana wa Timayo, Bartimayo, yule mwombaji kipofu, alikuwa ameketi kando ya njia. Naye aliposikia ya kwamba ni Yesu Mnazareti, alianza kupaza sauti yake, na kusema, Mwana wa Daudi, Yesu, Na wengi wakamkemea ili anyamaze, lakini alizidi kupaza sauti, Mwana wa Daudi, unirehemu.
Tazama zuio hilo lakini mara baada ya amri ya Yesu iliyowataka kumuita, hao hao ndio waliokuja kufanyika watiaji moyo wake, na hatimae kwa kukaza kwake, alipokea msaada au majibu yake! Jifunze sana kuwa, alipozuiliwa, hakuvunjika moyo, bali alizidi kuita!
Katika Mathayo tunauona mukutadha huu vyema, japo kuna kuonekana kuwa walikuwa wawili, ila nataka uuone huu mukutadha wa kutokukatishwa tamaa kiupana zaidi; “Mkutano wakawakaripia, wanyamaze. Lakini wao wakazidi kupaza sauti, wakisema, Uturehemu, Bwana, mwana wa Daudi.” 20:31 .
Tuendelee;
Yesu akasimama akasema, Mwiteni. Wakamwita yule kipofu, wakamwambia, Jipe moyo; inuka, anakuita. Akatupa vazi lake, akaruka, akamwendea Yesu. Yesu akamjibu, akamwambia, Wataka nikufanyie nini? Yule kipofu akamwambia, Mwalimu wangu, nataka nipate kuona. Yesu akamwambia, Enenda zako, imani yako imekuponya. Mara akapata kuona; akamfuata njiani.  

Mwanamke huyu ni kielelezo kikubwa sana cha kujifunza kwetu! Yesu alimpitisha katika vipimo kadha wa kadha na hatimae alishinda na yeye kuondoka na majibu yake! Kwa hiyo hupaswi kuvunjika moyo, uwe shujaa, maana tabia hiyo ndio ambayo Yesu anahiitaji kwako;
  Na tazama, mwanamke Mkananayo wa mipaka ile akatokea, akampazia sauti akisema, Unirehemu, Bwana, Mwana wa Daudi; binti yangu amepagawa sana na pepo. Wala yeye hakumjibu neno. Nao wanafunzi wake wakamwendea, wakamwomba, wakisema, Mwache aende zake; kwa maana anapiga kelele nyuma yetu. Akajibu, akasema, Sikutumwa ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.
Naye akaja akamsujudia, akisema Bwana, unisaidie. Akajibu, akasema, Si vema kukitwaa chakula cha watoto na kuwatupia mbwa. Akasema, Ndiyo, Bwana, lakini hata mbwa hula makombo yaangukayo mezani pa bwana zao. Ndipo Yesu akajibu, akamwambia, Mama, imani yako ni kubwa; na iwe kwako kama utakavyo. Akapona binti yake tangu saa ile.

Licha ya kujifunza swala la umuhimu wa kuwa na moyo usiokata tamaa kiwepesi na hata kukwazika kwa haraka, lakini pia lipo somo la kujifunza jingine, ambalo ni umuhimu au dhamani ama nguvu ya maombi ya hoja, kila hoja aliyoletewa kama kikwazo, aliipangua kwa maumakini!
Tunamuona Yesu akiisifia imani yake, ikiwa na maana kwamba pia unatakiwa kuhakikisha kiwango chako cha imani hakiyumbi pindi unapokuwa katika hali kama hii ya majibu yako kuonekana kana kwamba yamekawia mbele za Mungu!

Yapo mengi ndugu yangu ambayo ningeweza kuyanena ili kuzidi kukutia moyo, ila kwa hayo, nawiwa kukukumbusha kuhakikisha kwamba unazidi kukaza katika kumtazama Yeye, ambaye ndiye mwenye kukupatia majibu yako, haijalishi ni mwenzi wako au mwanandoa mwenzako amekuwa mwiba, ni mwenye hitaji la kuoa au kuolewa, uchumi ni mgumu, huduma haina mpenyo, yote katika yote fahamu sana kuwa utavuna kwa wakati ila kama hutazimia moyo, kwa hiyo usikubali kuzimia moyo.

Lakini pia kama hujaokoka, na unataka kuokoka, tafadhali fuatisha nami maneno haya ya sala ya toba, na fahamu sana kuwa wokovu sio dini mpya, bali ni kutengeneza na Bwana, ni kuishi maisha mapya yanayompendeza Mungu, ili hata ukifa leo uende mbinguni, na kumbuka nje ya wokovu hakuna kumuona Mungu, bali kuna adhabu ya moto wa jehanam wa milele, ni yangu rai kukuepushia adhabu hiyo, na kukusaidia kuingia katika Paradiso nchi au eneo lenye raha ya milele, ili umiliki, kufurahi, na kuishi pamoja na Mungu, tuwaone watakatifu huko kama wakina Ibrahimu, na Lazaro, na mitume, na manabii kama wakina Elian pia Heneko, Musa na wengine ambao yamkini walifanikiwa kuingia, kumbuka tena kuwa, nje ya hapo utaishi na Shetani milele, sasa epuka hili!

Sema; MUNGU BABA, NINAKUPENDA, ASANTE KWA KUNIPENDA KWANZA, LEO NIMETAMBUA KUWA MIMI NI MWENYE DHAMBI, NA NIPO TAYARI KUOKOOKA, TAFADHALI INGIA NDANI YANGU, SAMEHE DHAMBI ZANGU, NA FUTA JINA LANGU KATIKA KITABU CHA HUKU, NA ULIANDIKE SASA KATIKA KITABU CHA UZIMA WA MILELE, Ameni.

Kwa kufanya hiyo umekwisha kuokoka sasa, na tafadhali tafuta kanisa la watu waliokoka lililopo karibu nawe ukasali, hapo, waambie kuwa umeokoa hivi karibuni, ili wakulee vyema kiroho.
Mawasiliano yetu, kwa M-Pesa au Simu: +255 759 859 287, barua pepe: ukombozigospel@gmail.com
pia temnbelea: www.ukombozigospel.blogspot.com

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni