Alhamisi, 27 Februari 2020

JIFUNZE KUMTUMAINI BWANA.

Na Mwal Oscar Samba

“Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe” Mithali 3: 5.
Akili zako zinza mipaka, ufahamu wako kuna mahali unafikia ukingoni, utashi wako na upeo wako “ni-limited” nikiwa na maana kuwa kuna mahali unaishia, ila ukuu wa Mungu huvuka na ushinda ufahamu wote, ni yote katika yote.
“Je! Wewe hukujua? Hukusikia? Yeye Mungu wa milele, Bwana, Muumba miisho ya dunia, hazimii, wala hachoki; akili zake hazichunguziki.” Isaya 40:28.
Embu nenda name sanjari katika andiko hili; “Msijisumbue kwa jambo lo lote, bali katika kila jambo kwa kuomba na kusihi pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Nayo amani ya Mungu, inayopita fahamu/akili zote, itawalinda/hifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” Wafilipi 4.6-7.

Ina maana kwamba, unapokuwa taabuni, au katika adha, kitu kimoja wapo Mungu anachokifanya ni kuachilia Amani yake, ambayo huzidi akili zako, na ufahamu wako, ikiwa na mantiki kwamba ukiiruhusu ndani yako, akili yako au ufahamu wako utapata utulivu, na njia moja wapo ya kuiruhusu ni moja tu ambayo ni kuweka Imani na tumaini lako kwa Mungu, ni kweli tumeumbwa ili kutumia akili ila sio kuitegemea, wa kutegemewa au kutumainiwa ni Mungu pekee !

Kwa nini ? kwa sababu akili na uelewa wetu huwa na mipaka ! madakitari hutegemea akili zao, ufahamu na maarifa yao, wakishindwa watakwambai hapa hatuwezi, wanasheria au mawakili watakueleza kuwa hapa haiwezekani, mazingira ya uchumi au kiuchumi, ama mapito kwenye ndoa, au ugumu fulani unaweza kufikia mahali na kukueleza au kukwambia kuwa hili haliwezekani tena ! ni kweli na ni jibu zuri kabisa maana akili zetu zina mipaka!


Ila sivyo kwa Mungu, maana akili na ufahamu wake havichunguziki, alizifanya mbingu bila nguzo na kuzitundika hapo angani kama pazia, ameiwekea bahari mipaka na wala haijawai kuasi, ameliegesha jua na mwezi angani bila gundi, wala hakuna siku jua linaweza kuchelewa kuchomoza, wala kuzama !

Aliigawa bahari ya Shamu wana wa Israeli wakavuka, alilishimamisha jua kipindi cha Joshua na mwezi wana wa Israeli wakashinda vita kipindi kile !

Haijalishi mapito hayo ni kama maji mengi, wewe kumbuka tu hayata kugaharakisha kama Isaya 43 inavyoeleza, na kumbuka sana na fahamu kuwa hajasema hauta pitia hapo, la ! Bali amesema hayatakugarikisha, ikiwa na maana kuwa watapigana na wewe , ila kukushinda ndo hawawezi kukushinda !

Haijalishi mawimbi ni makubwa kiasi gani, maji ni mengi kwa kiasi gani, ila wewe mtazame Mungu, ukubwa au wingi wa maji hayo ni kwa ajili ya Mungu kujitwalia utukufu, kwa wewe kuvuka na adui zako kuzama, unaniuliza Mwali Oscar inakuaje ?

Jibu ni hili, maji kipindi cha Nuhu ndiyo yaliyowezesha safina ya Nuhu kuelea, bila maji isingeelea, lakini maji hayo hayo ndiyo yaliyowaua na kuwangamiza waliokuwa waovu siku zile !

Hujajua kuwa bila bahari ya Shamu wana wa Israeli bado wangeendelea kuteseka au kufuatwa-futwa na jeshi la Farao ? ukweli ni kwamba ni ndio !

Sasa nisikilize, maji yale yale yaliyogawanyika na  Mungu kujitwalia utukufu kwa kuwavusha wana wa Israeli, ndiyo hayo hayo yaliyojifunga na kuwameza wana wa Farao !

Sasa wewe waogopa nini ?
Jifunze tu kumtazama Bwana ! kwa hukuwahi kujifunza kwa Danieli na wenzie ?
Moto uliandaliwa kwa ajili yao, ndio uliotumika kuwamaliza adui zao ! sasa unadhania bila hivyo wale adui si wangezidi kuwatesa na kuwasumbua, pili hawa vijana bila hili pito unadhani wangeinuliwa kama kilichotokea ?

Na maamiri, na manaibu, na maliwali, na mawaziri, waliokuwa wamekusanyika pamoja, wakawaona watu hao, ya kuwa ule moto ulikuwa hauna nguvu juu ya miili yao, wala nywele za vichwa vyao hazikuteketea, wala suruali zao hazikubadilika, wala harufu ya moto haikuwapata hata kidogo. Nebukadreza akanena, akasema, Na ahimidiwe Mungu wa Shadraka, na Meshaki, na Abednego; aliyemtuma malaika wake, akawaokoa watumishi wake waliomtumaini, wakaligeuza neno la mfalme, na kujitoa miili yao ili wasimtumikie mungu mwingine, wala kumwabudu, ila Mungu wao wenyewe.  Basi mimi naweka amri ya kuwa kila kabila ya watu, na kila taifa, na kila lugha, watakaonena neno lo lote lisilopasa juu ya huyo Mungu wa Shadraka, na Meshaki, na Abednego, watakatwa vipande vipande, na nyumba zao zitafanywa jaa; kwa kuwa hakuna Mungu mwingine awezaye kuokoa namna hii.  Kisha mfalme akawakuza Shadraka, na Meshaki, na Abednego, katika wilaya ya Babeli.” Danieli 3:27-30

Nani ajuiaye kuwa jaribu hilo ni kwa ajili ya kukutukuza, au ni kwa ajili ya kukuinua ! ni kwa ajili ya kuwaaibisha adui zako na kumuinua Mungu wako ?

Najua moyoni mako unasema lakini Mwalimu hali ni ngumu, ndoa ni nzito, mwenzangu simuelewi, uchumi umekuwa mifupa mikavu ! “usiwe na shaka wewe itabirie tu !”

Uwemda moyoni mwako umefika mahali pa kushindwa kumuelewa Mungu ! wewe sio wa kwanza, hata Habakuki alisumbuliwa na hili, au alifika hapo, Daudi naye aliwahi kupitia hapo, kiasi cha kushangaa kuwa mbona waovu wanastawi na wenye haki kuteseka, hadi kufikia hatua ya kujifariji kuwa ni kama vile wanapaliwa mkaa ili wangaamie vyema !

Yesu pale msalabani alifikia mahali pagumu sana kiasi cha kusema Baba mbona umeniacha ! Hakika hayakuwa mazingira mepesi !

Lakini hakufikiria kuiacha Imani, hakufikiria kuukwepa msalabani, kama wewe unavyofikiria leo yamkini kujiua, kujinyonga, kumuacha Yesu !

Uwe kama Ayubu, ni kweli alipitia mahali pa gumu, ila hakuiacha Imani !
Najua umeomba, na kulitolea sadaka jambo hilo muda na muda sasa, ila usife moyo, majibu yako yapo, yanakuja, usione kama vile Mungu hakusikii, la, Hasha ! yu akisikia, tena sana, ila muda huu upo darasani, unapimwa, kama Ayubu, na punde utapokea majibu mema kama sura ya mwisho ya kitabu cha Ayubu ilivyo !

Binti mmoja alisema kuwa, mwaka huu ukipita kwa kweli kama bado sijaolewa, .. akija yeyote hata kama ni mlevi, mwisilamu, ..mimi twende tu ! hapana ndugu yangu, usifikie hapo !

Wachaga wa Rombo hupenda kusema kuwa, “usiache Yesu,” kweli kabisa, usikubali kumuacha Yesu kwa sababu kama hizo, wana heri wale wavumiliao majaribu, maana watapokea taji.

Wiki hii nilimpa binti yangu mmoja kazi ya kusoma kitabu cha Yakobo chote, na kumtaka kuwa akifikia kile kipengele cha kumtaka kuwa na uvumilivu kama mkulima akirudie mara baada ya kumaliza kitabu chote !

Mpendwa, hao walioshinda kwa uvumilivu, huitwa ni wenye heri au Baraka, maana walivumilia kama mkulima aingojavyo mvua ya mwisho ya mazao, nawe mngoje Bwana, mtumaini yeye, muhesabu yeye aliyekuaidia kuwa ni mwaminifu na siku moja yaja.

Ni kweli ulichokiomba kikikawia au kuchelewa moyo huugua, huumia, husononeka, lakini pia ni njia ya Mungu kukufundisha saburi  na kukupatia uthabiti wa moyo kama Warumi 5 isemavyo, ikiwa ni mtaji utokao kwa Yakobo moja, lakini kikipatika kilichongojewa moyo hufurahi, kama kwa Hana alivyompata Samweli, Sara hutuambia kuwa Bwana amemfanyia kicheko na kila atakayesikia atacheka pamoja naye, sasa nawe vumilia, na Bwana atakufanyia kicheko tu, haijalishi umri umeenda kwa kiasi gani, wewe mtazame Bwana !

Sijui wewe, ila mimi niliwahi kupitia mahali pagumu sana pa kukosa chakula, na andiko hili lilinitia moyo sana, maana nililisimamia, nawe najua lipo ambalo Bwana amekupa, nilisimamie hilo daima, ona langu;
“Mithali 10:3 Bwana hataiacha nafsi ya mwenye haki ife na njaa; Bali tamaa ya mtu mwovu huisukumia mbali.”

Mpendwa, ninakuitimishia na andiko hili, ambalo ndilo lilonipa mtaji wa waraka au makala hii, nilipolisikia darasani, moja kwa moja liliumbia ujumbe huu ndani yangu, maana kama umeweka tumaini lako kwenye duka, genge, au gari, siku likiungua moto, au kufilisika, ama kama ni kwenye elimu, siku ikipoteza dhamani machoni pa watoao ajira, au kama ni kwa mtu siku akifa, hakika uhusiano wako na Mungu utayumba tu !

Ni hatari kuuweka kwenye muda pia, kama wengine wafanyavyo, kuwa imechukuwa muda sana Mungu hajanijibu, ndio maaana nilikata tamaa ! nani alikwambia kuwa Mungu anafungwa na muda au na majira uyatakayo wewe ?

Andiko hili lina dhima nyeti sana, Zaburi 44: 6 Maana sitautumainia upinde wangu, Wala upanga wangu hautaniokoa.

Usitumaini maombi, mtumaini anayejibu maombi ! usitumainie sadaka, mtumainie aliyepokea sadaka !
Hatari kubwa ya leo ni hii, ukisikia mtu akisema kuwa nimeomba sana, nimefunga sana, nimekesha sana, lakini Mungu hajanijibu, kwa hiyo kaamua “kuacha Yesu,” maana yake aliweka tumaini kwenye maombi, sio kwa mjibu maombi, hajuia kuwa hata Daudi aliomba tena alikuwa kwenye dozi ya maombi ya siku 40 lakini Mungu hakumjibu, na bado mtoto alifariki.

Haimaanishi kuwa kuomba ni kubaya, ila shika hili sana, “Mungu atabaki kuwa Mungu, hata kama hajajibu maombi yako,” kujibu au kutokujibu hakumbadilishi Mungu, na maombi hayamlazimishi Mungu.
Sasa haina maana usiombe, la, Mathato 7:7-8, Yohana 15:7, kuna imizo la kuomba hapo ili upewe, kuomba ni kanuni ya kupokea, na ukiomba kwa bidii utapokea  kwa uzuri na ushindi  zaidi, kama hicho kitabu cha Yakobo 5 kisemavyo, kwa hiyo kufunga, kukesha ni njia njema sana, ila usiitegemee hiyo, mtegemee.

Pia Mungu hafungwi na muda, wala hatishiwi na mtazamo wako kimuda, sasa sio vibaya kuwa na muda moyoni mwako, maana imani ni kuwa na hakika, ila usijaribu kuutegemea muda, mtegemee Mungu katika huo muda, hili ni muhimu sana ili likuepushe kufikia walipofika wanaosema kuwa nimeomba sana, huu ni mwaka wa tatu sasa, nimengoja sana na sasa ninazeeka, ngoja niangalie njia nyingine, hawajui kuwa alijitwalia utukufu kwa Zakaria na mkewe, na Sara na mumwe wakiwa katika umri mkubwa !
Hajui kuwa YESU japo alitambua wito wake kabla ya kuzaliwa lakini alianza huduma akiwa na miaka 30, lakini Yeremia na Daudi walianza udogoni, na kuna mfalme katika Israeli aliatwana na maika 8, na alitenda vyema, sasa ukitaka kuiga sawa iga, lakini ujue kama sio majira ya Mungu utakwama tu, maana ni sawa na kujaribu kuendesha gari lisilo na nishati, ni kweli kwenye mteremko utatumia maji kama wengi wasemavyo, ila kilimani, tutajua tu umekwama !

Musa alianza huduma na miaka 80, sio kuanza tu, bali ndio alipokea wito rasmi, na alijijua ana wito akiwa na miaka 40, ila ilimchukuwa miaka mingine 40, sasa utaelewa ni kwa nini Mungu alimwambia Habakuki haya maneno; “3 Maana njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia.”

Haikuwa na maana kuwa Mungu hukawia la, tena ni la Hasha ! Maana Yeye hakawii, wala hachelewi, ila hufanya kazi yake kwa wakati, shida ni kwamba kwetu sisi huweza kuona kuwa amekawia, sasa hapo unaambiwa ingoje, lakini kiukweli haitakawia, na itafanya kazi kwa wakati wake, iliamriwa, sio utakayo iamuru wewe ?

Nenda kajiulize kuwa Yusufu ilibidi ipite miaka mingapi toka aote ile au zite ndoto, ndipo zije kutimia ? kumbuka aliota akiwa na miaka 17, nenda katazame aliovyoanza kutawala ! Au kuiwa malangoni pa Farao !
Nenda kwa Daudi, alikuwa kijana mdogo, wakati anapakwa mafuta, nenda katazame alianza kutawala Hebroni au Yerusalemi na miaka mingapi, kisha Israeli yote !
Wengi wanataka wakipokea ahadi ya Bwana leo, itimie leo au kesho, hilo haliwezekani, kuku akitaga leo, ni lazima asubirie yao la mwisho, ndipo yaje majira ya kutamia, kama ni kanga uwe na hakika kuwa atatamia mwezi mzima, kuku ni siku 21, tembo hubeba mimba kwa miezi mingapi ? unaonaje kama angetaka kubeba kwa siku 28 kama sungura ?

Hakika hata njiti asingezaa, na wengi katika mapito wamejikuta wakikumbwa na huu ugonjwa au hii shida, Daudi angeweza kufanya mapinduzi ya kijeshi, ili kuiharakisha ndoto yake, maana watu walimkubali, wengine walimfuata mapangoni, wakimuhudumia, na hata wapo walioimba na kumsifia Zaidi, lakini aliungoja wakati wa Bwana uliamriwa !

Ninayo mengi moyoni mwangu ila nikuachie hapo, ila nataka ujue kuwa niliwahi kumwambia binti mmoja, au niliwahi kuhubiri mahali kuwa, yamkini mumewe au mkeo, yupo chuo, sasa bado muda mdogo amalize, ukilazimisha kuolewa au kuoa leo, utajikuta unachukuana na asiye sahihi, kwa hiyo ungoje wakati wa Bwana.

Unajua kungoja kwa Daudi, kulimfanya kutiwa mafuta na wazee wa mji mara ya pili ? na ya tatu ? nakufundisha nini ? kuna hatari kama angejipaka mafuta mwenyewe, maana wenye mji wangekuwa hawajamkubali, leo hii tunahaha na kibali cha huduma lakini kwa kweli tumejitia mafuta wenyewe !

Ukienda kwa Yeyu ni kwamba alipokuwa anabatizwa ndipo Roho alipomshukia na kutamka kuwa huyu ndie mwana mpendwa na watu wamsikilize Yeye, unajua maaana yake ?

Hapo Roho alikuwa akimtia mafuta !

Sasa angelazimisha kabla ya wakati ni kwamba, hili lisingetokea, maana Yohana mbatizaji angekuwa hajaanza huduma bado, ni lazima ujuwe dhamani ya kuvumilia wakati ufike, maana Yohana wako ni lazima atangulie kwanza, sasa ukilazimisha kupita njia ambayo Yohana wako hajaisafisha uwe na hakika utakwama tu, ukitaka kuanza huduma bila kubatizwa au tukio la Roho kukupaka mafuta utakwa mtu, maana ili Roho aje ni lazima huduma ya Yohana iwepo kwanza.

Atakayekusemea kwa Farao wakati wake bado, sasa wewe vumilia, maaana yupo atakae kusemea, atakayae kutambulisha kwa Farao, kama Barnaba kwa mitume dhidi ya Paulo, leo wengi huhaha kujitambulisha wenyewe na sababu ni kwamba wameshindwa kuenenda na muda !

Wakulima hujua, hatari ya kuvuna matunda au mzao ambayo hayajakomaa, au kuiva vyema, sasa na wewe uwe makini, jifunze kumngoja Bwana, na huwezi kumngoja ambaye hujamtumaini, Zaidi ukipata kitabu chetu cha NGUVU YA KUMNGOJA BWANA, au cha USIFIE JANGWANI, visome, kuna jambo kubwa hapa utalipata, kipo pia cha FARAJA, USIOGOPE, JIPE MOYO na cha MTUMAINI BWAMA, pia kingne ni cha MTU WA NNE, au cha KATITAKATI YA SHIMO MTAZAME BWANA, asante na kwa heri.

Kama hujaokoka na unataka kuokoka, maana haii ni njia muhimu ya wewe kuweza kumngoja na kumtumaini Bwana, lakini pia itakuwezesha kuhakikisha ya kwamba unakuwa na uwepo wa kutosha wa Mungu, basi fuatisha sala hii;

Sema, MUNGU BABA, NINAKUPENDA, NIMETAMBUA YA KUWA MIMI NI MWENYE DHAMBI, NINAKUAMINI NA KUKUPOKEA MOYONI MWANGU KAMA BWANA NA MWOKOZI WA MAISHA YANGU, TAFADHALI FUTA JINA LANGU KWENYE KITABU CHA HUKUMU, NA ULIANDIKE KWENYE KITABU CHA UZIMA,AMENI.

Tafadhali sasa tafuta kanisa la watu waliokoka na ukasali hapo, wambie umeokoka na watakupa maelekezo maalumu, ameni, na hongera sana kwa hatua hiyo.

Kwa mawasiliano, au M-Pesa, 0759859287, Barua pepe: ukombozigospel@gmaoil.com

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni